Jumamosi, 6 Juni 2015

TAFSIRI YA KISAYANSI NA TEKNOLOJIA (TAFSIRI YA KIUFUNDI)



Kazi ya tafsiri haifanywi kiholela bali huzingatia baadhi ya hatua ili kufikiwa kiufanisi. Kwan kumrejelea Mwansoko (2006), anabainisha hatua zifuatazo:
Kwanza, mfasiri akabiliwapo na matini ya sayansi na teknolojia kwanza aisome kwa makini ili kuelewa maudhui yake. Lengo ni kufanya matini lengwa iakisi matini chanzi kiujumbe, zaidi ni kupigia mistari katika maneno magumu ili kuweza kuyatafutia maana katika vyanzo mbalimbali kama vile, kamusi ili kufanikisha zoezi la tafsiri.
Pili, ni kutathimini ubora wake.  Mfasiri anapaswa kuchunguza ubora wa matini chanzi, ili kuangalia kiwango chake cha urasimi yaani umaalumu kwa mfano; istilahi zilizotumika ni za kisayansi, mifano iliyotolewa inahalisika kisayansi, au mambo yanayoongelewa ni ya kisayansi. Jumla ya mambo haya yanatakiwa kuzingatiwa na mfasiri kwani yanathibitisha  uhai wa matini ya kiufundi.
Tatu, baada ya kuchambua matini yako ifasiri hasa kwa mkabala wa sentensi kwa sentensi. Mkabala huu unasisitizwa kwani unaeleweka zaidi kuliko wa neno kwa neno ambao kimsingi huweza kutuletea maana tenge katika tafsiri.
Nne, iweke tafsiri yako katika umbo linalotakiwa na mteja wako. Mfano; kama unafasiri kwa ajili ya shirika fulani la uchapishaji fuata mtindo wa machapisho ya shirika hilo kwa kuzingatia machapisho ya awali, na kama unafasiri gazeti au jarida fuata mtindo wa uandishi wake.
Baada ya kuangalia hatua za kufuata katika kufasiri matini za kisayansi na teknolojia, ufuatao ni mtindo wa lugha ambao mara nyingi hutumika katika kufasiri matini hizo:
Mwansoko (1994) na (2006), ameonesha mtindo wa lugha unaotumika katika tafsiri ya kiufundi (sayansi na teknolojia). Kwa kawida, lugha inayotumika katika tafsiri ya kiufundi huwa na lengo la kueleza usahihi na ukweli wa mambo yanayojadiliwa. Hivyo nia ya mwandishi hapo sio kusisimua au kuibua hisia au maono ya wale wanaomsoma au kumsikiliza, bali ni kutoa taarifa tu kama ilivyo. Lugha inayotumika katika tafsiri ya kiufundi kwa kawaida haina mhemko au jazba, ni ya msimamo wa katikati. Kutokana na sifa hizo tunapata mambo yafuatayo:
Hutumia sana kauli za kutendwa. Kauli hizi hutumika sana hata kama mwandishi ameandika kazi yake peke yake. Hii hutumika ili kuondoa dhana ya umilikishi katika uga wa taaluma.
       Mfano;  Masuala yaliyopendekezwa,
                     Jambo lililojadiliwa,
                     Imedhihirishwa,
                     Inapendekezwa,
                     Imekubaliwa n.k.
Jambo jingine ni matumizi makubwa ya vitenzi vya kidhahania. Vitenzi hivyo vya kidhahania ni vile ambavyo havioneshi au kubainisha waziwazi nafsi ya mtenda/mtendwa ama kubainisha mhusika. Matini za sayansi na teknolijia hazioneshi umiliki kama zifanyavyo za taaluma zingine kama fasihi.
        Mfano;  Kutembelea vikundi mbalimbali vya sanaa,
                      Kusoma tafsiri,
                     Ukimwi unaua chukua tahadhari.
Vilevile, ina matumizi makubwa ya nafsi ya kwanza wingi mahali pa nafsi ya kwanza umoja. Mtindo wa lugha katika tafsiri matini za kiufundi hukwepa matumizi ya nafsi ya kwanza umoja na badala yake hutumia nafsi ya pili wingi ikiwa na lengo la kufanya watumiaji wa matini ile kuamini kuwa imefanywa na watu wengi.
       Mfano;  Katika sura inayofuata tutachambua kwa undani zaidi mtindo wa kirasimi...
Mwansoko (1994:26) japo kitabu hichi kakiandika mwenyewe lakini katumia wingi.
                      Tunakubaliana na mawazo ya….
                       Tunazungumzia….
Kadhalika, hutumia sana kauli zisizoonyesha nafsi ya mtendaji. Hii inajidhihirisha pale ambapo mwandishi anakua kama amejitoa katika matini Fulani na kuonekana si muhusika kwa kuweka baadhi ya vipashio ambavyo havioneshi nafsi dhahiri. Hivyo tafsiri ya matini za kiufundi huwa na sifa hiyo.
        Mfano,   Imeafikiwa kuwa
                       Imeadhimiwa kwamba
                       Ilipendekezwa yafuatayo    
                       Inatazamiwa kwepo na…

Baada ya kuangalia mtindo wa lugha unaotumika katika matini za sayansi na teknolojia, sasa tuangalie sifa bainifu/upekee wa matini za sayansi na teknolojia kama ifuatavyo:
Kwanza, hazijigezi na utamaduni wowote. Hii ni kwa sababu matini hizi hutarajiwa kutumiwa na watu wote/ulimwengu mzima na hii ndio maana mara nyingi katika matini za kisayansi majina au istilahi huandikwa kama yalivyo bila kujali athari zake/ukali wa maneno hayo kwa utamaduni wa jamii fulani. Kwa mfano sehemu za mwili wa bianadamu mathalani uke, uume, puru, korodani nakadhalika huandikwa bayana bila kujali nani anapelekewa matini hizo, ana umri gani, heshima gani, au yuko katika muktadha upi. Mfano mzuri tunaweza kurejelea katika vitabu vya sayansi shule za msingi (darasa la sita) ambapo kuna michoro inayobainisha sehemu mbalimbali za mwili wa mwanadamu. Halikadhalika katika zana mbalimbali za kiufundi mfano katika karakana kuna kifaa kinachojulikana kama Mult-purpose spanner ambacho kwa Kiswahili kimetafsiriwa kama spana malaya. Hivyo kwa kiasi fulani kulingana na utamaduni wa waswahili kuna ugumu fulani katika kuzitaja au kuzirejelea zana au vifaa tajwa hapo juu, na wengine huona kuwa ni matusi.
Tafsiri za matini ya sayansi na teknolojia ina matumizi makubwa ya istilahi. Msokile, (1993) anaeleza kuwa, istilahi ni neno litumikalo kwa ufupi wa maneno mengi ya kiufundi kufuatana na ujuzi ama elimu maalumu. Kwa mfano, istilahi za fasihi, istilahi za kemia na jiografia. Katika uga wa sayansi kuna istilahi mbalimbali kama ifuatavyo:
Istilahi za Hisabati ni sphere, triangle, pai na algebra.
Istilahi za Baiolojia ni genetic, photosynthesis, nutrition na excretion.
Istilahi za Kemia ni calcium, element, potassium na carbonate.
Istilahi za Fizikia ni electric, current, ampere na voltage.
Katika istilahi, huwa kuna ugumu katika kupata au kutambua maana za istilahi mpya kwa mfasiri hasa zile ambazo hazifungamani sana na muktadha na hutokea mara moja tu katika matini. Mkabala ulio bora zaidi kwa matini ya kiufundi yenye istilahi nyingi za uvulivuli, ni kupigia mistari istilahi zinazoonekana kuwa ni za msingi wakati usomapo matini chanzi kwa mara ya kwanza na kisha tafuta maana zake kwenye kamusi. Istilahi hizo zinaweza kuwa na maana zaidi ya moja katika Nyanja moja ileile.
Wakati mwingine yawezekana ukakosa kabisa visawe vya istilahi za lugha chanzi katika lugha lengwa yako. Hali hii inapotokea mfasiri hulazimika kuunda istilahi zake mwenyewe kwa kutumia mbinu ambazo hutumiwa na lugha zote kuzalisha maneno mapya. Mbinu hizo ni pamoja na kutumia lugha lengwa yenyewe kwa minyumbuliko, miambatano, miungano, upanuaji wa maana za maneno yaliyopo na uhulutishaji.  Vilevile, mbinu ya kukopa kutoka lugha nyinginezo, lahaja, istilahi za kimataifa pamoja na tafsiri sisi.
Upekee wa mwingine wa tafsiri za kiufundi au za kisayansi na teknolojia, kwa kawaida huwa katika umbo la ripoti ya kiufundi, lakini yawezekana pia ikajumuisha vitabu vya rejea, maelekezo au notisi zinazoandikwa kwa kufuata mtindo wa maandiko ya kitaaluma. Hivyo upekee huu ndio unaoitofautisha matini ya kisayansi na matini zingine ambazo si za kisayansi. Na sifa hii ndiyo huweza kuitofautisha na matini nyingine kama za kifasihi, kisheria, kidini na zingine ambazo zinakuwa katika umbo la sentensi au katika aya ndefu, zisizokuwa katika mwonekano wa chati, grafu, orodha vielelezo, picha kama ilivyo katika ripoti. Hili limeshadadiwa katika ukurasa unaofuata. Pia, katika hoja ya kujumuisha vitabu vya rejea, kama kamusi, orodha ya istilahi na marejeo mengine ni muhimu katika tafsiri ya kiufundi kwa sababu kuna baadhi ya istilahi zinakuwa na maana zaidi ya moja. Kwa hiyo ni vyema kurejelea katika marejeo ili kupata maana mahususi ya istilahi inayoendana na muktadha husika. Kwa mfano; rejeleo lililoambatanishwa katika ukurasa unaofuata. Lakini pia mara nyingine, matini hizi za kiufundi huweza kuwa tu katika mfumo wa notisi au maelekezo ya kitaaluma kama vile, vitabu vya Baiolojia, Kemia, Jografia na taaluma zingine za kisayansi.
Upekee mwingine ni kuwa, tafsiri ya matini za kisayansi na teknolojia hutumia rejesta mbalimbali pamoja na kuonekana imeandikwa vibaya. Rejesta ni mtindo wa lugha inayotumika mahali penye shughuli maalumu inayotumiwa na kundi maalumu la wanajamii. Matumizi ya rejesta nyingi katika tafsiri hii hutokana na tafsiri hii kuwa na mada nyingi tofauti na tafsiri nyingine. Mfano katika vitabu vingi vya sayansi huwa na mada nyingi zilizochambuliwa tofauti na vitabu vya sanaa kama fasihi. Vilevile rejesta nyingi hutokana na mazoea ya watumiaji kama vile, mafundi magari, mafundi baiskeli, watu wa uhandisi na wengine. Kwa mfano fundi baiskeli hutumia rejesta kama vile;
Siti kava – kumaanisha sehemu anayokaa anayeendesha baiskeli
Stelingi – kumaanisha usukani
Breki – vifaa vya kufunga ili kupunguza mwendo
Sahanipeda – kifaa kama sahani ambacho hushika mnyororo
Medigadi – kifaa cha kukinga tope kinachopatikana katika gurudumu
Tairi – gurudumu


breki       filiwili                            kiti                           stelingi                                                                                                                                                                                                     
spoku Tairi (gurudumu)
                            gia                                 padeli                   
Rejesta na maneno yaliyofasiriwa hapo juu ni ya kisayansi na mwonekano wake na namna yanavyosikika katika lugha ya Kiswahili yanaonekana kutokuwa vizuri (hayavutii). Siyo hayo tu, pia hata katika simu tunazozitumia tafsiri ya maneno kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili zinaonekana kuwa na ukakasi huo huo uliojitokeza hapo juu. Kwa mfano;
Setting – mipangilio
Phone book – majina
Profile – mifumo
Alarm – kengele
Torch – taa          
Images – picha
Sms – ujumbe
Hiyo ni kwa mujibu wa shirika la simu linaloitwa Nokia.
Kwa  kuhitimisha tunaweza kusema kuwa, tafsiri ya sayansi na teknolojia ina upekee sana japo inakabiriwa na changamoto mbalimbali kama vile, ugumu wa upatikanaji wa istilahi za kisayansi na ugumu wa kupata maana za maneno au istilahi hizo za kisayansi na teknolojia. Hivyo changamoto hizo zinaleta shida katika tafsiri ya matini za sayansi na teknolojia.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni