Alhamisi, 25 Juni 2015


IDADI YA WAGOMBEA URAISI YAONGEZEKA
IDADI ya wagombea wanaochukua fomu kwa ajili ya kuwania kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) jana walifikia 39 baada ya mwanachama wake, Ritha Ngowi kuchukua fomu.
Ngowi, mkazi wa Dar es Salaam, anakuwa mwanamke wa tano kuchukua fomu, ambapo waliochukua fomu wa awali ni Balozi Amina Salum Ally, Waziri wa Katiba na Sheria Dk Asha-Rose Migiro, Dk Mwele Malecela na Monica Mbega.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari alisema yeye ni msomi ambaye ana shahada ya Maendeleo ya Jamii na pia amepitia kozi mbalimbali katika ngazi za diploma na cheti. Alisema vipaumbele vyake vitakuwa ni kwenye sekta ya elimu na uchumi.
“Nimeguswa sana na kuamua kugombea nafasi ya Urais lengo langu kubwa ni kutaka kuboresha elimu na Uchumi” alisema.
Alisema iwapo atachaguliwa kuwa Rais atahakikisha kila Mtanzania anapata elimu ya msingi na asiwepo Mtanzania asiye na uwezo wa kupata kipato na atahakikisha Watanzania wanawezeshwa ili kuwe na uzalishaji.
Kwa upande wa uchumi alisema atamairisha vivuko kwa ajili ya kupunguza foleni, na wakulima watapatiwa pembejeo na mazao yao yatatafutiwa masoko.
Hata wafanyabiashara kazi zao katika mazingira mazuri na wafanyakazi wa serikali watapata mishahara mizuri itakayowezesha wananchi kuishi maisha yenye viwango. Alisema atarekebisha mishahara kuanzia ngazi ya chini.
“Unaweza kuona mtu anapokea mshahara wa Sh 350,000 hadi 450,000 anapanga nyumba na analipa ada, maslahi yao lazima yarekebishwe,” alisema.
Alipohojiwa kama ana sifa 13 za mgombea wa CCM anavyo alisema anazo sifa hizo zote ndio maana amejitokeza. Pia alipohojiwa atatanuaje tatizo la rushwa iwapo ataingia madarakani, alisema ili kuondoa tatizo la rushwa jambo la kwanza ni kudhibiti vyanzo hivyo.
Alisema kutakuwepo na mikakati ili fedha zote zinazokusanywa zifike kwenye vyanzo husika na huduma zifike mahali panapostahili.
Katika historia yake alisema amewahi kufanya kazi Shirika la Uchumi na Maendeleo ya Wanawake Tanzania (Suwata) pia aliwahi kufanya kazi Chama cha Wasioona Tanzania, pia mmiliki wa shule ya sekondari ya Jostihego iliyopo Kibaha mkoani Pwani.
Mawaziri 2 warudisha fomu Wakati huo huo, mawaziri wawili wanaowania kuteuliwa na CCM, kuwa wagombea wa nafasi ya Urais jana walirudisha fomu. Waliorudisha fomu ni Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli na Waziri wa Kilimo na Ushirika Steven Wassira.
Balozi Karume Mgombea mwingine, Balozi Ally Karume alirejesha fomu yake saa 10.35 jioni. Alichukua fomu hiyo Juni 4, mwaka huu na kwenda kutafuta wadhamini katika mikoa mbalimbali ya Bara na Visiwani, mwenyewe akisema amepata wadhamini wa kutosha na wengine wa ziada.




 

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu amesema CCM ni chama pekee nchini ambacho kimefanikiwa na kinaendelea kupanua wigo wa demokrasia.
Nyalandu ni miongoni mwa wanachama wa chama hicho nchini waliotia nia ya kugombea nafasi ya urais katika uchaguzi ujao, aliyasema hayo jana wakati anazungumza na viongozi na wanachama wa CCM wilayani Masasi waliojitokeza kumdhamini.
Alisema hakuna tunu bora nchini zaidi ya kuendeleza umoja, amani na mshikamano uliopo hivi sasa ndani ya chama hicho huku akitoa mwito kwa wagombea wenzake ndani ya chama kuacha kukitia madoa chama na hata wao wenyewe, kwani kwa sasa CCM inahitaji umoja.
Alisema wana CCM nchini waondoe tofauti zao kwa kuwa ndiyo silaha pekee itakayoirudisha madarakani ambapo pia aliwaasa watanzania kupinga vitendo vyote vya kibaguzi, udini, ukabila na hata tofauti za rangi na kwamba endapo CCM kitampa ridhaa ya kuwa mgombea wa urais atahakikisha vitendo hivyo vinabaki kuwa historia.
Kwa mujibu wa Nyalandu, amekuwa CCM kwa muda mrefu sasa na kwamba kwa sasa Mungu ameruhusu kizazi kingine kipate fursa ya kuongoza nchi lengo likiwa ni kujenga uchumi imara kwa kutumia rasilimali zilizopo ikiwemo gesi, mafuta, milima pamoja na hifadhi za Taifa.

Jumamosi, 6 Juni 2015

TAFSIRI YA KISAYANSI NA TEKNOLOJIA (TAFSIRI YA KIUFUNDI)



Kazi ya tafsiri haifanywi kiholela bali huzingatia baadhi ya hatua ili kufikiwa kiufanisi. Kwan kumrejelea Mwansoko (2006), anabainisha hatua zifuatazo:
Kwanza, mfasiri akabiliwapo na matini ya sayansi na teknolojia kwanza aisome kwa makini ili kuelewa maudhui yake. Lengo ni kufanya matini lengwa iakisi matini chanzi kiujumbe, zaidi ni kupigia mistari katika maneno magumu ili kuweza kuyatafutia maana katika vyanzo mbalimbali kama vile, kamusi ili kufanikisha zoezi la tafsiri.
Pili, ni kutathimini ubora wake.  Mfasiri anapaswa kuchunguza ubora wa matini chanzi, ili kuangalia kiwango chake cha urasimi yaani umaalumu kwa mfano; istilahi zilizotumika ni za kisayansi, mifano iliyotolewa inahalisika kisayansi, au mambo yanayoongelewa ni ya kisayansi. Jumla ya mambo haya yanatakiwa kuzingatiwa na mfasiri kwani yanathibitisha  uhai wa matini ya kiufundi.
Tatu, baada ya kuchambua matini yako ifasiri hasa kwa mkabala wa sentensi kwa sentensi. Mkabala huu unasisitizwa kwani unaeleweka zaidi kuliko wa neno kwa neno ambao kimsingi huweza kutuletea maana tenge katika tafsiri.
Nne, iweke tafsiri yako katika umbo linalotakiwa na mteja wako. Mfano; kama unafasiri kwa ajili ya shirika fulani la uchapishaji fuata mtindo wa machapisho ya shirika hilo kwa kuzingatia machapisho ya awali, na kama unafasiri gazeti au jarida fuata mtindo wa uandishi wake.
Baada ya kuangalia hatua za kufuata katika kufasiri matini za kisayansi na teknolojia, ufuatao ni mtindo wa lugha ambao mara nyingi hutumika katika kufasiri matini hizo:
Mwansoko (1994) na (2006), ameonesha mtindo wa lugha unaotumika katika tafsiri ya kiufundi (sayansi na teknolojia). Kwa kawida, lugha inayotumika katika tafsiri ya kiufundi huwa na lengo la kueleza usahihi na ukweli wa mambo yanayojadiliwa. Hivyo nia ya mwandishi hapo sio kusisimua au kuibua hisia au maono ya wale wanaomsoma au kumsikiliza, bali ni kutoa taarifa tu kama ilivyo. Lugha inayotumika katika tafsiri ya kiufundi kwa kawaida haina mhemko au jazba, ni ya msimamo wa katikati. Kutokana na sifa hizo tunapata mambo yafuatayo:
Hutumia sana kauli za kutendwa. Kauli hizi hutumika sana hata kama mwandishi ameandika kazi yake peke yake. Hii hutumika ili kuondoa dhana ya umilikishi katika uga wa taaluma.
       Mfano;  Masuala yaliyopendekezwa,
                     Jambo lililojadiliwa,
                     Imedhihirishwa,
                     Inapendekezwa,
                     Imekubaliwa n.k.
Jambo jingine ni matumizi makubwa ya vitenzi vya kidhahania. Vitenzi hivyo vya kidhahania ni vile ambavyo havioneshi au kubainisha waziwazi nafsi ya mtenda/mtendwa ama kubainisha mhusika. Matini za sayansi na teknolijia hazioneshi umiliki kama zifanyavyo za taaluma zingine kama fasihi.
        Mfano;  Kutembelea vikundi mbalimbali vya sanaa,
                      Kusoma tafsiri,
                     Ukimwi unaua chukua tahadhari.
Vilevile, ina matumizi makubwa ya nafsi ya kwanza wingi mahali pa nafsi ya kwanza umoja. Mtindo wa lugha katika tafsiri matini za kiufundi hukwepa matumizi ya nafsi ya kwanza umoja na badala yake hutumia nafsi ya pili wingi ikiwa na lengo la kufanya watumiaji wa matini ile kuamini kuwa imefanywa na watu wengi.
       Mfano;  Katika sura inayofuata tutachambua kwa undani zaidi mtindo wa kirasimi...
Mwansoko (1994:26) japo kitabu hichi kakiandika mwenyewe lakini katumia wingi.
                      Tunakubaliana na mawazo ya….
                       Tunazungumzia….
Kadhalika, hutumia sana kauli zisizoonyesha nafsi ya mtendaji. Hii inajidhihirisha pale ambapo mwandishi anakua kama amejitoa katika matini Fulani na kuonekana si muhusika kwa kuweka baadhi ya vipashio ambavyo havioneshi nafsi dhahiri. Hivyo tafsiri ya matini za kiufundi huwa na sifa hiyo.
        Mfano,   Imeafikiwa kuwa
                       Imeadhimiwa kwamba
                       Ilipendekezwa yafuatayo    
                       Inatazamiwa kwepo na…

Baada ya kuangalia mtindo wa lugha unaotumika katika matini za sayansi na teknolojia, sasa tuangalie sifa bainifu/upekee wa matini za sayansi na teknolojia kama ifuatavyo:
Kwanza, hazijigezi na utamaduni wowote. Hii ni kwa sababu matini hizi hutarajiwa kutumiwa na watu wote/ulimwengu mzima na hii ndio maana mara nyingi katika matini za kisayansi majina au istilahi huandikwa kama yalivyo bila kujali athari zake/ukali wa maneno hayo kwa utamaduni wa jamii fulani. Kwa mfano sehemu za mwili wa bianadamu mathalani uke, uume, puru, korodani nakadhalika huandikwa bayana bila kujali nani anapelekewa matini hizo, ana umri gani, heshima gani, au yuko katika muktadha upi. Mfano mzuri tunaweza kurejelea katika vitabu vya sayansi shule za msingi (darasa la sita) ambapo kuna michoro inayobainisha sehemu mbalimbali za mwili wa mwanadamu. Halikadhalika katika zana mbalimbali za kiufundi mfano katika karakana kuna kifaa kinachojulikana kama Mult-purpose spanner ambacho kwa Kiswahili kimetafsiriwa kama spana malaya. Hivyo kwa kiasi fulani kulingana na utamaduni wa waswahili kuna ugumu fulani katika kuzitaja au kuzirejelea zana au vifaa tajwa hapo juu, na wengine huona kuwa ni matusi.
Tafsiri za matini ya sayansi na teknolojia ina matumizi makubwa ya istilahi. Msokile, (1993) anaeleza kuwa, istilahi ni neno litumikalo kwa ufupi wa maneno mengi ya kiufundi kufuatana na ujuzi ama elimu maalumu. Kwa mfano, istilahi za fasihi, istilahi za kemia na jiografia. Katika uga wa sayansi kuna istilahi mbalimbali kama ifuatavyo:
Istilahi za Hisabati ni sphere, triangle, pai na algebra.
Istilahi za Baiolojia ni genetic, photosynthesis, nutrition na excretion.
Istilahi za Kemia ni calcium, element, potassium na carbonate.
Istilahi za Fizikia ni electric, current, ampere na voltage.
Katika istilahi, huwa kuna ugumu katika kupata au kutambua maana za istilahi mpya kwa mfasiri hasa zile ambazo hazifungamani sana na muktadha na hutokea mara moja tu katika matini. Mkabala ulio bora zaidi kwa matini ya kiufundi yenye istilahi nyingi za uvulivuli, ni kupigia mistari istilahi zinazoonekana kuwa ni za msingi wakati usomapo matini chanzi kwa mara ya kwanza na kisha tafuta maana zake kwenye kamusi. Istilahi hizo zinaweza kuwa na maana zaidi ya moja katika Nyanja moja ileile.
Wakati mwingine yawezekana ukakosa kabisa visawe vya istilahi za lugha chanzi katika lugha lengwa yako. Hali hii inapotokea mfasiri hulazimika kuunda istilahi zake mwenyewe kwa kutumia mbinu ambazo hutumiwa na lugha zote kuzalisha maneno mapya. Mbinu hizo ni pamoja na kutumia lugha lengwa yenyewe kwa minyumbuliko, miambatano, miungano, upanuaji wa maana za maneno yaliyopo na uhulutishaji.  Vilevile, mbinu ya kukopa kutoka lugha nyinginezo, lahaja, istilahi za kimataifa pamoja na tafsiri sisi.
Upekee wa mwingine wa tafsiri za kiufundi au za kisayansi na teknolojia, kwa kawaida huwa katika umbo la ripoti ya kiufundi, lakini yawezekana pia ikajumuisha vitabu vya rejea, maelekezo au notisi zinazoandikwa kwa kufuata mtindo wa maandiko ya kitaaluma. Hivyo upekee huu ndio unaoitofautisha matini ya kisayansi na matini zingine ambazo si za kisayansi. Na sifa hii ndiyo huweza kuitofautisha na matini nyingine kama za kifasihi, kisheria, kidini na zingine ambazo zinakuwa katika umbo la sentensi au katika aya ndefu, zisizokuwa katika mwonekano wa chati, grafu, orodha vielelezo, picha kama ilivyo katika ripoti. Hili limeshadadiwa katika ukurasa unaofuata. Pia, katika hoja ya kujumuisha vitabu vya rejea, kama kamusi, orodha ya istilahi na marejeo mengine ni muhimu katika tafsiri ya kiufundi kwa sababu kuna baadhi ya istilahi zinakuwa na maana zaidi ya moja. Kwa hiyo ni vyema kurejelea katika marejeo ili kupata maana mahususi ya istilahi inayoendana na muktadha husika. Kwa mfano; rejeleo lililoambatanishwa katika ukurasa unaofuata. Lakini pia mara nyingine, matini hizi za kiufundi huweza kuwa tu katika mfumo wa notisi au maelekezo ya kitaaluma kama vile, vitabu vya Baiolojia, Kemia, Jografia na taaluma zingine za kisayansi.
Upekee mwingine ni kuwa, tafsiri ya matini za kisayansi na teknolojia hutumia rejesta mbalimbali pamoja na kuonekana imeandikwa vibaya. Rejesta ni mtindo wa lugha inayotumika mahali penye shughuli maalumu inayotumiwa na kundi maalumu la wanajamii. Matumizi ya rejesta nyingi katika tafsiri hii hutokana na tafsiri hii kuwa na mada nyingi tofauti na tafsiri nyingine. Mfano katika vitabu vingi vya sayansi huwa na mada nyingi zilizochambuliwa tofauti na vitabu vya sanaa kama fasihi. Vilevile rejesta nyingi hutokana na mazoea ya watumiaji kama vile, mafundi magari, mafundi baiskeli, watu wa uhandisi na wengine. Kwa mfano fundi baiskeli hutumia rejesta kama vile;
Siti kava – kumaanisha sehemu anayokaa anayeendesha baiskeli
Stelingi – kumaanisha usukani
Breki – vifaa vya kufunga ili kupunguza mwendo
Sahanipeda – kifaa kama sahani ambacho hushika mnyororo
Medigadi – kifaa cha kukinga tope kinachopatikana katika gurudumu
Tairi – gurudumu


breki       filiwili                            kiti                           stelingi                                                                                                                                                                                                     
spoku Tairi (gurudumu)
                            gia                                 padeli                   
Rejesta na maneno yaliyofasiriwa hapo juu ni ya kisayansi na mwonekano wake na namna yanavyosikika katika lugha ya Kiswahili yanaonekana kutokuwa vizuri (hayavutii). Siyo hayo tu, pia hata katika simu tunazozitumia tafsiri ya maneno kutoka Kiingereza kwenda Kiswahili zinaonekana kuwa na ukakasi huo huo uliojitokeza hapo juu. Kwa mfano;
Setting – mipangilio
Phone book – majina
Profile – mifumo
Alarm – kengele
Torch – taa          
Images – picha
Sms – ujumbe
Hiyo ni kwa mujibu wa shirika la simu linaloitwa Nokia.
Kwa  kuhitimisha tunaweza kusema kuwa, tafsiri ya sayansi na teknolojia ina upekee sana japo inakabiriwa na changamoto mbalimbali kama vile, ugumu wa upatikanaji wa istilahi za kisayansi na ugumu wa kupata maana za maneno au istilahi hizo za kisayansi na teknolojia. Hivyo changamoto hizo zinaleta shida katika tafsiri ya matini za sayansi na teknolojia.

MWALIMU MWANAFUNZI (USHAIRI)

NA RICHARD, KASHINJE 0764711129
rkashinje@gmail.com

MWALIMU MWANAFUNZI

1          Mwalimu uwe makini, makini kumakinika
Mwalimu si masikini, akilize kulabuka.
Walimu sikilizeni, yamoyo yalotukuka
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo.

2          Siku uwapo kazini, kusoma huna kikomo
Hata kama nimezani, kitabu hakina komo
Pata yawanazuoni, mapya kwako yaliyomo
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo

3          Usishike mazoea, kusoma moja pekee
Kusema umebobea, hakika si wapekee
Kazi yako watachukua, waliosoma pekee
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo


4          Usipokuwa msomi, tena wakusoma sana
Wanafunzi hawakusomi, kwako ni aibu sana
Hawatakupenda msomi, na hiyo fedheha sana
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo

5          Kumbuka ile kauli, ambayo kwetu nirai
Mwalimu kuwa mkali, wanafunzi kuzirai
Kwako murua kauli, kwao somo wafurai
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo




6          Siku zimebadilika, yakupasa utambue
Wanafunzi huzunguka, ukweli wautambue
Yakupasa kumakinika, wasomi wasiumbue
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo.

7          Msomi tulikuamini, tuakukabidhi kazi
Kwakuwa niutamaduni, nzuri ufanyapo kazi
Pia tuanatatumaini, kazi iota mizizi
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo

8          Kusoma hana kikomo, mwalimu ni mwanafunzi
Mwanafunzi hana komo, kusoma ni mwanafunzi
            Haya ndani yawe yamo, kazi ni uwanafunzi
Mwalimu ni mwanafunzi, kusoma hana kikomo


Mashairi ya kiswahili

USHAIRI WA KISWAHILI
HAKI
1          Maisha haya jamani, kweli niipatashika
Maisha kama majani, kweli yanapukutika
Maisha yalo gizani, leo yaanasikika
Haki yamtu jamani, hakika nipatashika.

2          Tuliishi kwaamani, tena kwakujiamini
Haki zetu mikononi, wote tulizitieni
Lakini wetu karani, leo twamzikeni
Haki ya mtu jamani, hakika nipatashika.

3          Kila mnyonge nyumbani, wote walifurahia
Swahibu kwake moyoni, kwake alipigania
Amani kwetu moyoni, wote tulisherekea
Haki ya mtu jamani, hakika nipatashika.

4          Kichwa chake chahekima, busara zimesimama
 Kelo za watu mapema, tayari kuzitazama
Waume na kinamama, haki hawakulalama
Haki ya mtu jamani, hakika nipatashika.

5          Tuliishi kwa matao, busara yake karani
Karani wetu mtwao, sote twaweka kirini
Twakukumbuka wanao, leo hii korokoroni
Haki ya mtu jamani, hakika nipatashika.

6          Mungu ulo mbinguni, sikia hiki kilio
Mjalie wetu karani, korokoroni kilio
Wote tunamdhamini, twomba tena kwakilio
Haki ya mtu jamani, hakika nipatashika.

NA RICHARD, KASHINJE 0764711129

rkashinje@gmail.com

MIIKO YA KABILA LA WAKEREWE

Falsafa nidhana nyeti sana katika maissha  na utamaduni wa wabantu waishio katika bara la Afrika. Katika kujadili swali hili tutaanza kujadili dhana za Falsafa jinsi ilivyoelezwa na wataalamu mbalimbali, tutaleleza maana ya miiko jinsi ilivyoelezwa na vyanzo mbalimbali, tutaeleza historia fupi ya wilaya ya Ukerewe, tutaeleza kiini cha swali letu ambapo tutakeleza miiko mbalimbali ambayo inapatikana katika kabila la Wakerewe na hatimaye tutahitimisha kwa kutoa tathimini ya miiko hiyo kwa sasa jinsi inavyochukuliwa. Tuanze kwa kuziangalia maana mbalimbali za Falsafa jinsi ilivyojadiliwa na wataalamu mbalimbali kama ifuatavyo;
http://sw.wikipedia.org/wiki/Falsafa Falsafa ni jaribio la kuelewa na kueleza ulimwengu kwa kutumia akili inayofuata njia ya mantiki kwa kuchunguza mambo kama kuweko na kutokuweko, ukweli, ujuzi, uzuri, mema na mabaya, lugha, haki na mengine yoyote.
http://pengotz.blogspot.com/2007/12/falsafa-ya-elimu-tanzania.html wanaeleza kuwa, falsafa ni taaluma inayojishughulisha na kutafuta ukweli wa jambo kwa njia ya kutafakar.
Kwa ujumla tunaweza kuseama kuwa, Falsafa ni tawi la sanaa ambalo linajishughulisha na kutafuta ukweli wa mambo jinsi yalivyo kwa njia ya fikra na tafakuri za hali ya juu juu ya mambo hayo ambayo ni ukweli, mantiki, kuwepo na kutokuwepo kwa mambo.
Baada ya kueleza maana ya Falsafa jinsi ilivyoelezwa hapo juu sasa tuziangalie maana za  miiko jinsi zilivyojadiliwa navyanzo mbalimbali kama ifuatavyo;
en.wikipedia.org/wiki/Taboo Miiko ni makatazo makali ya matendo yaliyo katika imani ya tabia ambayo pengine ni takatifu sana au laana sana kwa mtu binafsi wa kawaida kufanya chini ya tishio ya adhabu isyo ya kawaida. (tafsiri yetu)
www.wisegeek.com/what-is-a-taboo.htm  Mwiko ni kukataza dhidi ya shughuli fulani, kwa kawaida mizizi katika imani za kitamaduni au maadili. Vitu, watu, na maeneo pia inaweza kama mwiko ilivyoelezwa, kwa maana ya kuwa wao ni haramu au kwamba sheria maalum zinazowazunguka wao.
www.oxforddictionaries.com/definition/english/taboo Miiko kijamii au kidini na desturi ni kukataza au kuzuia vitendo fulani au akipinga kushirikiana na mtu fulani, mahali, au jambo.
Hivyo, miiko ni makatazo ambayo jamii huyaweka na kuyatilia adhabu kali kwa mtu yeyote ambaye angeweza kukaidi maagizo hayo.
Baada ya kumaliza kueleza maana ya miiko sasa tuiangalie historia ya wilaya  ya Ukerewe  ambamo ndimo miiko yetu tuliyoijadili ndimo ilimotoka kama ifuatavyo;
https://envaya.org/lakevictoriachildren_lvc/history wanaeleza  kuwa, Ukerewe ni kisiwa kubwa katika Ziwa Victoria ambacho ni kubwa ya kitropiki na ni cha  pili kwa ukubwa  katika maziwa yenye maji baridi  duniani. Kisiwa hiki kina ukubwa wa eneo la 6400 km2.  nchi kavu ina  640 km2 ni nchi na wengine 5760 km2 ni maji ya Ziwa Victoria Kuna visiwa 38 kisiwani Ukerewe kambapo makao makuu yake ni wilaya ya  Nansio . Kati ya visiwa 38, visiwa 15 ni ya kudumu na hutumika kwa makazi wakati vinavyobaki hutumika kama makazi yamda kwa wavuvi . Wilaya iko kusini mwa Wilaya Ilemela na Magu. Mashariki kuna Wilaya  Bunda na Musoma katika Mkoa wa Mara, kwa kusini magharibi inapakana na Wilaya ya Sengerema, kwa magharibi mkoa wa Kagera na kaskazini Jamhuri ya Kenya na Uganda
baada ya kumaliza kueleza historia ya wilaya ya ukerewe ifuatayo ni miiko inayopatikana katika wilaya ya ukerewe katika kabila la wakerewe.
1)      Nimarufuku kwa mtoto wa kiume kukaa jikoni, maana yake ni kuwa, nguo za mama yake zinaweza kuvuka akaona uchi wa mama yake. Lakini maana yake halisi ni kuwa kama mtoto wa kiume angekaa jikoni angeliweza kuunguo
2)      Nimarufuku kuua chatu. Maana yake kwani ni unauugua bila kupona na hadi kufa. Lakini ni kwamba chatu alikuwa amefugwa na mtemi wa wakerewe.
3)      Nimarufuku mwanamke kutaja baba mkwe wake kwa jina lake au jina linalofanana na la baba mkwe wake. Maana yake ni kutunza heshima na badala yake mwanamke alitafta tafsida ya jina hilo ndiopo amuite baba mkwe wake.
4)      Nimarufuku kwa mtu yeyote kuanza kuchimba kaburi la mtualiyefariki  mwenye magonjwa  kama kifafa, kichaa mpaka ndugu yake aanza kuchimba ndipo wengine wafuatie. Hii ikikiukwa watu hao watauugua  mpaka kufa. Na suluhu yake ni kwamba mazindiko hufanywa ili kuhakikisha marehemu anazikwa na magonjwa yake.
5)      Nimarufuku kwa bibi harusi kukatisha katikati ya uwanja wa kaya. Hii ni kwa sababu katikati ya uwanja ndipo baba nyenywe nyumba alipokuwa akiotea moto kwa hiyo angeliweza kumuona akiwa uchi.
6)      Nimwiko kwa mwanamke aliyeolewa kula na baba mkwe wake meza moja.  Hii ilikuwa ni kwa sababu wanaume wanakula haraka na wanawake wanakula taratibu hivyo waliogopa mkwe wao kutokushiba.
7)      Nimwiko kwa mwanamke kula nyama ya kuku au mayai yake kwa kuogopa kuwa watoto wangekuwa na tabia za kula kila kaya. Lakini maana yake ya ndani ni kuwa; kwakuwa wakerewe ni wafugaji  wa kuku kwahiyo waliogopa kuku wao kumalizwa na mama wakati wa ujauzito.
8)      Nimarufuku kwa  mtoto yeyote kukalia kinu kama akikalia kinu hatakua lakini maana yake ni kwamba ikiwa mtoto akikalia kinu angeweza kutoa ushuzi na hatimaye kuchafua kinu ambacho ni chombo cha kutwangia nafaka.
9)      Nimarufuku kwa mwanaume kula na mama mkwe wako. Kwani angweza kumlaza njaa lakini maana yake ni kwa nguo za mama mkwe wake zingeweza kuanguka na kumuona uchi wake.
10)  Nimarufuku kwa wanaume katika familia kula meza moja na wanawake kwani nguo zingaliweza kuanguka na kuwaona dada zake na mama zake uchi. Lakini ni kwamba mwanamke anakula taratibu na mwanaume anakula haraka haraka hivyo waliogopa kuwalaza njaa wanawake.
11)  Nimarufuku kwa mkerewe kula ndege aina ya nfunzi kwani ataugua ugonjwa wa kuvuka ngozi ya juu na ngozi ya ndani kuja juu. Lakini maana yake ni kuwa kwa kuwa ndege huyo alikuwa natumika katika kufanyia shughuli za kiganga hivyo waliogopa kuruhusu ndege hao wasilike ili wasije wakaisha mana hata upatikanaji wake ni adimu sana.
Kwa kuhitimisha tunaweza kutoa tathimini ya miiko hiyo na jinsi ilivyo kwa sasa. Mpaka kufikia mwanzoni mwa miaka ya tisini miiko ilikuwa bado ina mashiko na ilikuwa ikifanya kazi na watu waliieheshimu. Lakini baada ya kuingia kwa maendeleo ya sayansi na teknolojia yaliyosukumwa na utandawazi miiko mingi ya wabantu imekufa kwa kuwa mambo siku hizi yanapelekwa kizungu na kwa hali hii kuna hatari ya miiko kufa na kupotea kabisa . hivyo juhudi za ziada zinahitajika sana ili kuweza kuzilithisha katika vizazi vijavyo kwa kuanzisha miradi mbalimbali ya kuandika miiko ili kuzitunza kwa mstakabali wa maisha ya baadaye.


MAREJELEO
http://pengotz.blogspot.com/2007/12/falsafa-ya-elimu-tanzania.html imepakuliwa tarehe 13/04/2015 saa 4:48 asubuhi
en.wikipedia.org/wiki/Tabo  imepakuliwa tarehe 14/04/2015 saa 2:16 usiku

http://sw.wikipedia.org/wiki/Falsafa. Imepakuliwa tarehe 13/04/2015 saa 4:18 asubuhi